Home VIWANDANISHATI PURA yatakiwa kuendelea kuvutia wawekezaji utafutaji mafuta na gesi

PURA yatakiwa kuendelea kuvutia wawekezaji utafutaji mafuta na gesi

0 comment 36 views

Serikali imeielekeza Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) kuendelea kuvutia  uwekezaji katika vitalu vilivyo wazi vya mafuta na gesi asilia ili kuongeza kiasi cha nishati hiyo nchini.

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga ametoa maelekezo hayo Februari 19, 2025 Wilayani Morogoro, Mkoa wa Morogoro wakati akifungua kikao cha Baraza la wafanyakazi wa PURA kinacholenga kujadili  masuala mbalimbali ikiwemo Mpango na Bajeti ya Taasisi hiyo kwa mwaka  wa fedha 2025/26.

“Mkifanikiwa  kuvutia uwekezaji katika shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi, nchi itaongeza ugunduzi wa rasilimali hiyo muhimu ikiwa ni pamoja na kuogeza futi za ujazo wa gesi  inayopatikana nchini.

Pia mkiendelea kuvutia uwekezaji kupitia Duru ya Tano ya kunadi vitalu itakayozinduliwa mwezi Machi mwaka huu, pamoja na faida zilizopo, mtakuwa mmeendeleza jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuendelea kuifungua Tanzania kiuchumi na kuvutia uwekezaji Zaidi,” amesema Kapinga.

Amesema Wizara ya Nishati inatambua umuhimu wa tukio la Duru ya Tano ya kunadi vitalu vya utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini pamoja na kutambua kazi kubwa ambayo imeshafanyika kuelekea uzinduzi wa tukio hilo ambalo amesema kuwa ni muhimu katika
kuvutia uwekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini.

“Kwa muda mrefu sasa tumekuwa tukizungumzia ugunduzi wa futi za ujazo trilioni 57.54 pekee ni wakati sasa wa kufanya zaidi na zaidi ili tuweze kuongeza ugunduzi wa rasilimali hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa,” amesisitiza Kapinga

Katika kikao hicho cha  Baraza la wafanyakazi,  ameupongeza uongozi wa PURA kwa kuendelea kuwashirikisha watumishi wake katika kujadili, kupanga na kupitisha mipango na Bajeti ya Taasisi kwenye Baraza la Wafanyakazi ikiwa ni utekelezaji pia wa Sheria ya Majadiliano ya Pamoja katika Utumishi wa Umma.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter