Home BIASHARAUWEKEZAJI Tanzania imesajili miradi ya Dola Bilioni 8.65 ndani ya mwaka mmoja

Tanzania imesajili miradi ya Dola Bilioni 8.65 ndani ya mwaka mmoja

0 comment 30 views

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ndani ya mwaka mmoja, Serikali imefanikiwa kusajili miradi 9,678 yenye thamani ya dola za Marekani milioni 8,658 hali ambayo inaonesha matokeo chanya ya uwekezaji nchini.

Waziri Mkuu ameeleza hayo Septemba 11, 2024 wakati akizungumza na wadau mbalimbali walioshiriki hafla ya uzinduzi wa Taarifa tano za Maboresho ya Mazingira ya Biashara na Uwekezaji na Nyenzo za Usimamizi wa Uwekezaji nchini iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizindua Taarifa tano za Maboresho ya Mazingira ya Biashara na Uwekezaji na Nyenzo za Usimamizi wa Uwekezaji nchini iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

“Miradi 9,678 yenye thamani ya dola za Marekani milioni 8,658 ilisajiliwa mwaka 2023 ikilinganishwa na miradi 8,401 yenye thamani ya dola za Marekani milioni 5,558.47 iliyosajiliwa mwaka 2022,” amesema.

Akifafanua kuhusu taarifa ya kwanza ya uwekezaji ya mwaka 2023 ambayo inaonesha takwimu za matokeo chanya ya uwekezaji nchini, Waziri Mkuu amesema miradi hiyo imeweza kuzalisha ajira za moja kwa moja 195,803 ikilinganishwa na ajira 76,841 zilizozalishwa mwaka 2022.

Akielezea juhudi zilizofanywa na Serikali kwenye mipango ya maendeleo ya uwekezaji wa sekta ya umma na sekta binafsi, pamoja na mazingira ya biashara, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kufanya mageuzi ya uendeshaji na usimamizi wa Taasisi na Mashirika ya Umma ili kuhakikisha kwamba yanaendeshwa kwa ufanisi na tija katika kuwahudumia wananchi.

“Suala hili tayari limetolewa maelekezo na Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Agosti 28, 2024 katika kikao kazi cha Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Mashirika ya Umma na Taasisi za Serikali.

Hivi sasa, Serikali imeridhia mapendekezo ya kutungwa kwa Sheria ya Uwekezaji wa Umma itakayoimarisha na kuweka masharti bora ya usimamizi wa uwekezaji katika Mashirika ya Umma pamoja na kuwa na vyanzo vya uhakika vya fedha kwa ajili ya uwekezaji.”

Amesema Serikali imeendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ikiwemo Ujenzi wa Mfumo wa Kielektroniki wa Kuhudumia Wawekezaji unaoitwa Tanzania Electronic Investment Window (TeIW) ili kumwezesha mwekezaji kusajili mradi ndani au nje ya nchi na kupata vibali vya uwekezaji ndani ya siku tatu iwapo ametimiza vigezo.

“Awamu ya kwanza ya ujenzi wa mfumo huu imekamilika na imewezesha kuunganishwa kwa mifumo ya taasisi saba ambazo ni Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Idara ya Uhamiaji, Idara ya Kazi, Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA); Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC),” ameeleza Waziri Mkuu.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amezitaka taasisi na mamlaka za Serikali ziharakishe marekebisho ya sheria ambazo zinachangia urahisi wa kufanya biashara ili kuhakikisha kwamba sheria mpya zinawezesha mazingira bora ya biashara na uwekezaji.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter