Home VIWANDANISHATI Bilioni 688 zawekezwa Stiegler’s Gorge

Bilioni 688 zawekezwa Stiegler’s Gorge

0 comment 79 views

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Doto James amethibitisha kuwa malipo ya awali ya Shilingi bilioni 688.7 yamekabidhiwa kwa Mkandarasi wa mradi wa kufua umeme wa maji katika maporomoko ya Mto Rufiji maarufu kama Stiegler’s Gorge uliopo mkoani Pwani.

James, amesema kuwa malipo hayo yamekabidhiwa kwa kampuni  ya Arab Contractors (Osman A Osman & Co and Elsewedy Electric S.A.E. (JV AC – EE) ya Misri, ikiwa ni asilimia 70 ya asilimia 15 ya gharama zote zitakazotumika kutekeleza mradi huo mkubwa wa umeme ambao unatarajiwa kujengwa kwa muda wa miezi 36 na baada ya kukamilika kuzalisha takribani megawati 2,115.

“Kukamilika kwa mradi wa Mto Rufiji kutakuwa ni kichocheo muhimu katika kuiwezesha Tanzania kufikia azma ya kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 kutokana na kuwepo kwa umeme wa uhakika na wakutosha utakaosaidia maendeleo ya uchumi wa viwanda na maendeleo endelevu ya wananchi kwa ujumla”. Amesema Katibu Mkuu huyo.

Imeelezwa kuwa kutakuwa na ajira zipatazo 100 za wataalamu ambao watashughulikia kituo baada ya ujenzi na ajira kwa wananchi itaongezeka kutoka 4,500 hadi 6,000.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dk. Hamis Mwinyimvua ameeleza kuwa Aprili 15 mwaka huu, benki za CRDB na UBA kwa pamoja walitoa dhamana ya malipo ya awali na kuwezesha utekelezaji wa mradi huo wa Sh. 6.6 trilioni. Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Dk. Alexander Kyaruzi ameipongeza serikali kwa kutoa fedha ili kuwezesha ujenzi wa mradi huo ambao amedai una faida kubwa kwa taifa kuanza.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter