Home BIASHARAUWEKEZAJI Harakisheni kusikiliza kesi za biashara: Rais Samia

Harakisheni kusikiliza kesi za biashara: Rais Samia

0 comment 323 views

Rais Samia Suluhu Hassan amezitaka mahakama nchini kuharakisha kusikiliza kesi za kibiashara.

Rais Samia amesema hayo wakati akihutubia maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika kwenye viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Februari 01, 2023.

Amesema ni vema mahakama ikatoa kipaumbele cha kuharakishwa usikilizwaji wa kesi za kibiashara katika masuala ya kisheria pindi inapotokea migogoro ili kuvutia mitaji na uwekezaji na kufungua fursa za biashara.

“Tunapovutia mitaji na uwekezaji nchini na kufungua fursa za kibiashara tunatambua kwamba uwekezaji huambatana na maswala ya kisheria na migogoro ya kibiashara. Ni vema mahakama zetu kutoa umuhimu kwa mashauri ya aina hiyo pia,” amesema Rais Samia.

Ameitaka Wizara ya Katiba na Sheria pamoja na wadau wa usuluhishi kubainisha maeneo yanayotakiwa kufanyiwa kazi ikiwemo kutunga sera ya usuluhishi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na Jaji Mkuu wa Tanzania Prof. Ibrahim Hamis Juma wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ambayo Kitaifa yamefanyika katika viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma 01, Februari, 2024.

Aidha, Rais Samia amesema ni wakati muafaka wa kujielekeza kufanya utatuzi kwa njia ya usuluhishi bila kufungwa na masharti ya kiufundi yanayokwamisha kutenda haki.

Ameitaka Wizara hiyo kushirikiana na wadau kutekeleza kikamilifu utoaji wa msaada wa kisheria kwa kuzingatia Ibara ya 107A ya Katiba inayowataka kutenda haki kwa wote bila kujali hali zao za kijamii au kiuchumi.

Vile vile, Rais Samia amesema mitazamo ya wadau wa Mahakama nchini haina budi kujielekeza kwenye kupunguza muda unaotumika kwenye mashauri ili wananchi watumie muda wao mwingi kwenye uzalishaji mali.

Amebainisha kuwa serikali inafanya jitihada kuimarisha upatikanaji wa huduma za kisheria kwa wananchi wasio na uwezo kupitia Mama Samia Legal Aid Campaign kwa kuwa kuna uhitaji mkubwa wa msaada wa kisheria nchini.

Kampeni hiyo tayari imewafikia wananchi 383,293 katika Mikoa 6 ya Dodoma, Manyara, Shinyanga, Ruvuma, Simiyu na Singida ambapo imeweza kutatua migogoro takribani 511.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiwa pamoja na viongozi mbalimbali wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ambayo Kitaifa yamefanyika katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma Februari 01, 2024.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter