Home HABARI ZA AFRIKA MASHARIKI Vivutio nyanda za juu Kusini vitangazwe: Majaliwa

Vivutio nyanda za juu Kusini vitangazwe: Majaliwa

0 comment 85 views

Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana nyanda za juu kusini.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo alipotembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii sehemu ya TANAPA kwenye maonesho ya 30 Nane Nane yanayoendelea katika viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya.

Waziri Mkuu amebainisha kuwa filamu ya Royal Tour imeleta hamasa kwa watalii wengi kumiminika nchini hivyo ni jukumu la Wizara kutangaza vivutio vyote vinavyopatikana nchini na kutokuegemea upande mmoja tu.

“Utalii ukifunguka sekta ya kilimo na mifugo itapata mwamko na kukua zaidi. Nilipokuwa nchini Urusi nilipata muda wa kuongea na balozi wetu nchini Urusi moja ya jambo alilonieleza ni shirika la Ndege la Urusi liko mbioni kuanzisha safari za moja kwa moja kuja nchini Tanzania.”

Akimkaribisha Waziri Mkuu, Kamishna msaidizi wa uhifadhi Theodora Aloys amesema kwamba wao kama wahifadhi wanachangia kilimo kwa kiasi kikubwa kwani wanahifadhi misitu pamoja na vyanzo vya maji vilivyomo katika misitu hiyo.

Ameongeza kuwa shughuli za uhifadhi wa vyanzo vya maji vinavyopatikana nyanda za Juu kusini husaidia katika shughuli za kiuchumi kwani vyanzo hivi ndio chanzo kikuu cha uzalishaji wa umeme katika mabwawa ya Mtera na Kidatu pamoja na ujazaji wa maji katika Mradi wa Ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter