Home KILIMOKILIMO BIASHARA Vyama vya ushirika vyatakiwa kujiendesha kibiashara

Vyama vya ushirika vyatakiwa kujiendesha kibiashara

0 comment 76 views

Vyama vya ushirika vya wakulima wa mazao mbalimbali vimetakiwa kujiendesha kibiashara ili kukuza uchumi wa ushirika na kujenga vyama imara vyenye kushiriki kwenye ushindani wa kibiashara.

Naibu Waziri wa Kilimo Anthony Mavunde ameyasema Juni 14, 2023 wakati wa uzinduzi wa Programu ya Taasisi ya WE EFFECT ya ‘Livehoods and Right to Food Program’ (LRF) jijini Dodoma, ambapo moja ya vipaumbele vya Program hiyo ni maendeleo ya vyama vya Ushirika.

“Kufuatia mpango wa Serikali wa kukuza Kilimo kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030, Serikali imeweka mkakati wa kuimarisha maendeleo ya ushirika, kuhakikisha wakulima wananufaika na vyama vya ushirika na kuchangia kwenye sekta ya kilimo bila kuwepo na ubabaishaji,’ amesema Mavunde.

Ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kuwa Sekta ya Kilimo inakua na mkulima ananufaika.

“Hivyo Ushirika ninaotamani kuuona ni ule ushirika ambao utakuwa imara na ambao utashiriki moja kwa moja kwenye mnyororo wa uongezaji thamani wa mazao ya kilimo badala ya kuendelea kubaki wakusanyaji wa mazao ya wakulima.

Tumechoka kusikia ubadhirifu na sifa mbaya ya ushirika, tunataka sasa tuone ushirika imara utakaochochea uchumi wetu kwa kujenga viwanda vya kuchakata mazao ya kilimo chini ya usaidizi mkubwa wa Benki ya Taifa ya Ushirika,” amesisitiza Mavunde.

Amesema dhana nzima ya ushirika sio mbaya, ni watu wachache tu ndio wanataka kuichafua tasnia hii kwa kufanya kazi bila weledi na uaminifu.

Amebainisha kuwa serikali kupitia ofisi ya Mrajisi wa Vyama vya Ushirika itaendelea kuchukua hatua stahiki za kisheria kwa wale wote ambao watadiriki kuichafua tasnia hiyo.

Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika Mashariki wa WE EFFECT George Onyango amesema programu hii yenye gharama ya Tsh 9.3 bilioni inajielekeza katika mikoa nchini na hasa katika maeneo ya ardhi na makazi, Maendeleo ya Vyama vya Ushirika, mazingira na ushiriki wa vijana na wakina mama kwenye sekta ya kilimo.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter