Zaidi ya leseni 4,000 zipo katika utaratibu wa kutolewa katika maeneo manne ya Mkoa wa Kimadini Mbogwe mkoani Geita, huku wazawa na wawekezaji kutoka nje wakitakiwa kuchangamkia fursa zilizopo mkoani humo.
Akizungumza katika mahojiano, Afisa Madini Mkazi wa Mbogwe, Mhandisi Jeremiah Hango amesema maeneo yaliyotengwa ni Nyamikonze ambapo leseni 81 ziliweza kugawiwa kwa wachimbaji wadogo, kuna eneo la Mwamakiliga leseni 27 zilitengwa.
“Maeneo mengine ni Bukombe kijijini leseni 140 na sasa hivi mchakato wa Kigosi ambapo takribani leseni 4,000 kutengwa,” amesema Mhandisi Hango.
Amesema zoezi la ugawaji bado linaendelea na kwamba fursa zilizopo zikitumiwa vizuri serikali itaweza kukusanya kiasi kikubwa cha maduhuli.
“Nawakumbusha wamiliki wa leseni ambao wameshikilia leseni katika mkoa wetu wa kimadini Mbogwe wazifanyie kazi leseni hizo, nyingi hawazifanyii kazi, kuna leseni za utafiti ambapo ukienda saiti watu wanaofanya utafiti ni wachache sana.
Vile vile niwakumbushe kama leseni hizo hawatazifanyia kazi tutazifuta na kuwapa watu wengine wenye nia ya kufanyia kazi leseni na sio kuzishikilia,” amesema.
9