Home BIASHARA Mitandao ya kijamii na fursa kiuchumi

Mitandao ya kijamii na fursa kiuchumi

0 comment 164 views

Matumizi ya mitandao ya kijamii yamekuwa sana kila kona duniani. Ni moja ya njia ya kupashana habari kwa kasi. Watu mbalimbali hususani vijana ndio kundi kubwa linalotumia mitandao hiyo ikiwemo Facebook, Twitter, Whatsapp, Youtube, Instagram na mingine mingi.

Vijana wengi wamekuwa wakiitumia kufanya mijadala mbalimbali hususani siasa na mambo mengine. Ni wachache walioweza kuona fursa katika mitandao hiyo ya kujiingizia kipato kwa namna moja ama nyingine.

Wafanyabiashara sasa wameanza kutumia kurasa mbalimbali za mitandao yao kutangaza biashara zao. “Ni kweli, nimenufaika sana na mitandao ya kijamii katika kutangaza biashara yangu ya sabuni,” anasema kijana Adrew Mpambazi ambae ni mfanyabiashara wa sabuni za kuogea zijulikanazo kama The Champ Mpambazi.

Mpambazi anasema kazi yake yeye ni kuandika na kuonesha sabuni zake katika mitandao ya kijamii na huko ndiko anapopata wateja wake wengi.

“Ninachofanya mimi ni kuposti bidhaa zangu, sina duka popote, nikipata mteja nawapelekea walipo, tofauti na kukaa dukani kusubiri wateja. Hii inanisaidia sana na niwashauri vijana wenzangu watumie hii mitandao kukuza uchumi wao, inalipa,” anasema Mpambazi .

Anaongeza kuwa hiyo ni njia rahisi kutokana na kuwa yeye bado ni mjasiriamali mdogo inapunguza gharama za kupanga pango la duka.

Kwa sasa ambapo teknolojia inazidi kukua kwa kasi ni vema vijana wakatumia fursa zilizopo hususani kwenye mitandao ya kijamii kujiletea maendeleo badala ya kufanya soga pekee.

Vijana wengi hususani watu maarufu wanatumia mitandao kuonesha kazi zao ikiwemo bidhaa na vitu vingine vingi na kujipatia wateja, ingawaje pia kuna utapeli na udanganyifu unafanywa na baadhi ya watumiaji wa mitandao hiyo, hivyo ni vema tahadhari zikachukuliwa mapema.

Wateja wengi sasa wanakwenda madukani/sokoni kununua bidhaa wakijua zinapopatikana bila kuzunguka zunguka.

 

 

 

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter