Home KILIMOKILIMO BIASHARA Wanunuzi wa korosho wapewa siku nne

Wanunuzi wa korosho wapewa siku nne

0 comment 61 views

Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema serikali imetoa muda wa siku nne kwa wanunuzi waliojiandikisha kununua korosho kupeleka barua katika Ofisi ya Waziri Mkuu wakiweka wazi kiasi cha tani wanazohitaji na muda watakaozichukua. Majaliwa amesema hayo jijini Dodoma wakati akitoa tamko la serikali kuhusu ununuzi wa zao la korosho.

“Hivyo wanunuzi waliojiandikisha wakiwemo na wale wote ambao wamekuwa wananunua kwenye minada lakini kwa kiasi kidogo, wahakikishe ndani ya siku hizo nne kuanzia leo Ijumaa hadi Jumatatu saa 10 alasiri wawe wameleta barua na ofisi yangu ipo wazi saa 24. Mwenye nia ahakikishe katika siku hizo nne iwe ndio mwisho wa kununua korosho na waandike barua kwani ofisi yangu ipo wazi saa 24 wana nafasi ya kuleta barua wakati wowote wakionyesha nia yao na kiwango wanachokihitaji. Zaidi ya hapo serikali haitoruhusu kampuni yoyote kununua korosho tena” . Amefafanua Waziri Mkuu.

Aidha, Waziri Majaliwa amesema serikali imeshuhudia kusua kwa minada kwenye msimu wa ununuzi wa korosho wa mwaka huu, hali iliyopelekea wao wakiongozwa na Rais Magufuli kukutana na wanunuzi wa korosho na kukubaliana kununua kwa bei inayoanzia Sh. 3,000 na kuendelea.

“Mjadala ulikuwa wa wazi na wafanyabiashara wenyewe walipendekeza bei ambayo ilikuwa inaanzia Sh. 3,000 hata hivyo baada ya kikao hicho ununuzi katika minada imeendelea kusuasua na hata tani zilizokuwa zikinunuliwa zilikuwa kidogo sana. Sisi tunaiona hali hii kama mgomo baridi ambao si sawa sana kwani malengo yetu sisi na sekta binafsi ni kumfanya mkulima apate bei nzuri”. Ameeleza Majaliwa.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter