Home KILIMO Serikali ya Tanzania na mikakati kuongeza uzalishaji wa pareto

Serikali ya Tanzania na mikakati kuongeza uzalishaji wa pareto

0 comment 287 views

Serikali imesema inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuongeza uzalishaji wa zao la pareto kutoka tani 3,150 mwaka 2022/2023 hadi tani 4,238 mwaka 2023/2024.

Hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 121 ya lengo la kuzalisha tani 3,500.

Aidha, kilo 5,130 za mbegu bora za pareto zimesambazwa katika msimu wa 2023/2024 kwa wakulima 10,260 wa pareto katika mikoa sita inayolima zao hilo ambayo ni Mbeya, Iringa, Songwe, Njombe, Manyara na Arusha sambamba na mafunzo ya kilimo bora kwa wakulima 2,530.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Kilimo David Silinde wakati akijibu swali la Yustina Arcadius Rahhi Mbunge wa Viti Maalum Bungeni jijini Dodoma, Aprili 22, 2024.

Silinde ameeleza kuwa Viwanda vya kuchakata maua ya pareto vimeongezeka kutoka viwanda viwili (2) vilivyokuwepo mwaka 2020/2021 hadi viwanda nane (8) mwaka 2022/2023 vinavyowezesha uongezaji wa thamani na kupanua wigo wa masoko ya pareto na bidhaa zake.

Ameeleza kuwa Serikali imeanza kushirikiana na Kampuni ya Pareto Tanzania (PCT) kuanzisha shamba la ekari 300 katika Wilaya ya Makete kama sehemu ya utekelezaji wa mpango wa kuanzisha mashamba makubwa.

Awali akijibu swali la Mbunge wa Mlimba, Godwin Emmanuel Kunambi kuhusu ujenzi wa mradi wa umwagiliaji katika Bonde la Mto Kilombero, Silinde amesema mwaka 2023/2024, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inaendelea na upembuzi yakinifu na usanifu wa kina (feasibility study & detailed design) wa miradi ya umwagiliaji katika bonde hilo.

“Mwaka 2016 Serikali ilifanya upembuzi yakinifu wa awali wa miradi ya umwagiliaji katika bonde la Kilombero lenye ukubwa wa hekta 53,344 ambapo skimu za Kisegese, Udagaji, Mgungwe na Mpanga – Ngalamila zilihusishwa katika kazi hiyo.

Upembuzi yakinifu wa awali ulibaini kuwa kuendelezwa kwa skimu hizo kutanufaisha kaya 15,102 na kutoa ajira 69,476” ameeleza.

Aidha, amesema mwaka 2023/24 Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika skimu za Kisimiri Juu na Kisimiri Chini zenye ukubwa wa hekta 802.

Vilevile, skimu za Kyamakata, Ukombozi, Ngabobo, Mapama, Momela, Mwakeny, Olkung’wado, Kimosonu, Eyani, Maktemu na Oldonyo Wass.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter