Kilimo biashara kinaendelea kukua barani Afrika na muda umefika kwa watu hususani vijana kuchagamkia fursa mbalimbali zinazotokana na kilimo.
Watu wengi ambao wamefanikiwa bado wanaendelea kuzichangamkia fursa za kilimo biashara kwa sababu wanajua zina mafanikio makubwa na muda unavyozidi kwenda, teknolojia zinavyoendelea kuboreshwa kilimo biashara kitafanyika kwa urahisi zaidi.
Hata watu waliofanikiwa tayari wanachangamkia kilimo biashara. Tajiri Aliko Dangote ameshawekeza mamilioni ya fedha katika utengenezaji wa mpunga, kilimo ambacho kinalipa sana.
Hivyo zifuatazo ni sababu zitakazokuhamasisha kuwekeza katika kilimo biashara barani Afrika:
Ardhi
Ni rahisi kupata ardhi kwa bei nafuu Afrika hususani maeneo ya vijijini ambapo ardhi huuzwa kwa bei nafuu.
Soko
Idadi ya watu duniani inaendelea kukua kadri muda unavyokwenda hivyo suala la masoko linarahisishwa. Afrika peke yake hutumia mabilioni ya fedha kila mwaka kuagiza chakula kutoka nje wakati uwezekano wa kuzalisha ndani upo. Wajasiriamali wanaweza kutumia fursa hii hivyo kuzalisha vyakula vinavyoagizwa nje na kuuza kwa bei rahisi. Pia viwanda mbalimbali hutegemea malighafi zinazotokana na kilimo hivyo watu hususani vijana wanaweza kuchangamkia fursa hiyo.
Teknolojia
Teknolojia mbalimbali zinaendelea kutengenezwa na kufika barani Afrika. Uoga wa watu wengi kuhusu kufanya kilimo ni teknolojia watu wengi wanaona ni sekta ngumu hasa pale inapowabidi kutumia mifumo ya kizamani.
Lakini siku zinavyozidi kwenda hata serikali za nchi za Afrika zinaendelea kutafuta njia rahisi zaidi zinazoweza kuwahamasisha wananchi wao kufanya kilimo. Serikali ya Tanzania imekuwa ikitoa elimu kuhusu kilimo biashara na badala ya watu kulima maeneo makubwa na kupata mazao kidogo, sasa programu mbalimbali zimekuwa zikiandaliwa ili kuwafundisha wakulima kilimo cha kisasa kwa kutumia nguvu ndogo. Programu hizo zimekuwa zikitolewa kwa wafugaji pia. Hivyo kujenga mikakati na kuhakikisha una uzoefu wa teknolojia za kisasa ni baadhi ya mambo yatakayokusaidia kunufaika na uwekezaji huu.
Mtaji
Ni rahisi kuanza na mtaji wowote katika kilimo. Watu wengi wametoa ushuhuda kuhusu jinsi walivyoanza na mitaji midogo hadi kupata mafanikio makubwa. Suala la mtaji isiwe sababu kuu ya kutochangamkia fursa zilizopo katika kilimo biashara. Pia ikiwa huna kabisa mtaji unaweza kuomba mkopo katika taasisi mbalimbali za fedha ambazo zimejikita kuwakomboa wakulima wadogo.
Ajira
Ikiwa bado unawaza sekta ya kuwekeza na kutoa ajira kwa watu wengine, kilimo biashara ni sekta ambayo inaendelea kuwa sababu kubwa ya ajira na mafanikio. Watu wengi hukimbilia katika kilimo kama ajira. Hapa Tanzania zaidi ya 70% ya wananchi ni wakulima. Sekta hii inachangia 58% ya ajira na 27% ya Pato la Taifa.
Kadri muda unavyokwenda Afrika inaendelea kubadilika, watu wanaendelea kuelimika na kufanya mambo makubwa. Ili kwenda sawa ni muhimu kuchagamkia fursa zinazojitokeza na kwenda sawa na mabadiliko yanayoendelea kutokea duniani.