Home BIASHARA Mikopo 10% yasubiri majibu ya Rais Samia

Mikopo 10% yasubiri majibu ya Rais Samia

0 comment 231 views

Mbunge wa viti maalum Mwantumu Zodo ametaka kufahamu ni lini Serikali itarejesha mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri ambayo imesitishwa kwa muda mrefu.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma Februari 02, 2023 amehoji “kwa kuwa wakina mama bado wanahangaika na mikopo ya kausha damu mitaani, je ni lini sasa serikali itaanza tena zoezi hili la utoaji mikopo ili kuondoa adha kwa wakina mama wa mkoa wa Tanga na Tanzania kwa ujumla?”.

Pia ametaka kujua kama bado Halmashauri zinaendelea kutenga fedha hizo.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Deogratius Ndejembi amesema Waziri amekwishawasilisha ripoti yake na kumkumbusha Rais Samia Suluhu Hassan ili mchakato wa utoaji wa mikopo hiyo urejee.

Ndejembi amesema “na hivi tunavyozungumza Mheshimiwa Spika Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI amekumbushia kwa Mheshimiwa Rais hili jambo ili liweze kurudi sasa na kuuanza utekelezaji wake , kama kuna sheria ya kubadilika iletwe mbele ya Bunge hapa ili sheria hizo ziweze kubadilika”.

Ameongeza kuwa kwa mujibu wa sheria ya fedha ya Serikali za mitaa, halmashauri zinaendelea kutenga fedha hizo za mikopo na endapo mikopo hiyo itatakiwa kutolewa fedha zipo.

Utoaji wa mikopo hiyo ya halmashauri ilisitishwa baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kupokea ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kuelekeza mapitio ya namna mikopo hiyo inavyotolewa.

About Us

PesaTu ni kitengo cha habari cha MediaPix ambacho huandika makala za biashara na uchumi wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Waasisi wa kampuni wana uzoefu mkubwa kwenye tasnia ya habari na mawasiliano wakiwa kwenye fani hio tangu mwaka 1905.

Editors' Picks

Newsletter