Na Mwandishi wetu
Baada ya mazungumzo baina ya Rais John Pombe Magufuli na Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi kufanyika jana Ikulu jijini Dar es salaam, Tanzania na Misri zimefikia makubaliano ya kibiashara yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 878 sawa na trilioni 1.9 za kitanzania.
Serikali ya Misri na Tanzania pia zimekubaliana kuwa na mazungumzo juu ya matumizi ya Mto Nile ili kuhakikisha kwamba nchi zote mbili zinafaidika na mto huo ambao chanzo chake kikubwa cha maji ni Ziwa Victoria.
Makubaliano mengine yaliyofikiwa baada ya ugeni huo ni pamoja na kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, elimu, ulinzi na usalama, utalii pamoja na kupambana dhidi ya rushwa na dawa za kulevya.
Akielezea kuhusu sekta ya afya, Rais Magufuli amesema nchi hizi mbili zimekubaliana kuongeza wataalamu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na pia kupeleka wataalamu zaidi visiwani Zanzibar. Hadi kufikia 2020 Misri wameahidi kuwezesha kufanyika kwa operesheni za figo hospitali ya Muhimbili.
Naye kwa upande wake, Rais wa Misri amesema Tanzania na nchi yake zitaendelea kubadilishana wataalamu katika miradi mbalimbali na amemshukuru mwenyeji wake Rais Magufuli kwa jitihada zake za kuleta amani na kupambana na ufisadi. Al Sisi pia amesisitiza nchi za Afrika kudumisha ushirikiano.
Discussion about this post